Alhamisi, 13 Machi 2014

WATATU WASHIKILIWA NA JESHI LA POLISI KAGERA

 Moses Augustine ,Muleba,13,3,2014


JESHI la polisi mkoani Kagera linawashikilia watu watatu akiwemo mchungaji wa kanisa la Chochea moto, Elmes Fabian,kwa tuhuma za kufanya uharifu, kufyeka mashamba ya migomba na kuvunja nyumba 3 za wakazi wa kijiji cha Kishulo wilayani Muleba wakiwatuhumu kuwa ni wachawi.

Tukio hilo limesababisha wananchi zaidi ya 12 wakiwemo watoto na wanafunzi wa shule za msingi kukosa makazi huku wazazi wao wakilazimika kukimbilia kwenye taasisi ya kusaidia wazee na yatima ya "Kwa Wazee" iliyopo kata ya Nshamba ili kupata hifadhi ya muda.

Kamanda wa polisi mkoa wa Kagera, George Mayunga,amethibitisha kuwepo kwa tukio hilo na kudai kuwa watu watatu akiwemo mchungaji wa kanisa la Chochea moto(Emba Omulilo) wanashikiliwa kwa kosa la kuchochea vurugu,kudhuru miili na kuharibu mali kinyume cha sheria.

Amesema uchunguzi wa jeshi hilo umebaini baadhi ya wananchi wakiwemo watoto wa watuhumiwa hao wa ushirikina walifanya ukatili huo wakishirikiana na baadhi ya wananchi waliokuwa na lengo la kuwaua wazee wa familia hizo.

Kamanda Mayunga amewataja walionusurika kuuawa kuwa ni Fabian Albert na mkewe Gaudensia Fabian,Methodia Leonard na Geogina Kayonga wote wakazi wa kijiji cha Kashulo wilayani humo mkoani kagera.

Mchungaji wa kanisa la Chochea Moto(Emba Omulilo) anadaiwa kuwahubiri waumini wake kuwa anauwezo mkubwa wa kuwabaini wachawi ambao wamekuwa wakisumbua kijijini humo kabla ya kuanza kuwataja kwa majina.

Hatua hiyo ilionekana kupokelewa kwa hisia kali na waumini wake wakiwemo watoto wa watuhumiwa, hivyo kuungana na wananchi wengine kwenda kuharibu mali na kuwadhuru wazee hao kwa mapanga.

Mratibu wa shirika lisilokuwa la kiserikali la "Kwa Wazee" Lydiah Lugazia,amesema kutokana na ukatili huo kwa wazee hao wamelazimika kuwachukua na kuwahifadhi kwa muda ili kunusuru maisha yao kufuatia wananchi kutaka kuwaua kwa imani potofu za kishirikina.

Aidha msaada huo ni wa siku chache huku akiitaka serikali kuweka mazingira mazuri kwa walioathiliwa na ukatili huo kutafuta ufumbuzi wa kuwalejesha katika maneo yao na kuimalisha ulinzi ili waendelee na shughuli zao za uzalishaji mali.

Kwa Upande wake Ofisa miradi wa asasi hiyo,Edmund Revelian,ameiomba serikali kuacha kusajili makanisa kinyemela kwa kuwa baadhi ya viongozi wa dini wamekuwa wakichochea vurugu kwa jamii kutokana na maslahi yao binafsi.

Kadhalika ameonyesha kushangazwa na jamii kuamini sana imani za kishirikina ambazo kwa kiwango kikubwa zimekuwa zikiwakumba wananchi maskini,huku wengine wakitumia nafasi hizo kutaka kupokonya mali za wengine iwapo watafanikiwa kuwatimua kutoka kijijini humo.

Kwa upande wao watuhumiwa wa vitendo hivyo vya kishirikina walipoulizwa na gazeti hili kuhusiana na tuhuma dhidi yao walikanusha vikali na kudai huo ni mpango kabambe ambao umesukwa kitambo na watoto wao ili wafanikiwe kutwaa mashamba na nyumba za wazazi wao.

Wamesema kabla ya tukio hilo,watoto wao wamekuwa wakiwatishia kuwaua iwapo hawatakuwa tayari kuwapa mashamba iliwauze na kupata pesa za kufanya mambo yao.

Kutokana na hali hiyo Mkuu wa mkoa wa Kagera,Kanali mstaafu Fabian Masawe,ametumia nafasi hiyo kuwaonya wananchi wote mkoani humo ambao wamekuwa na tabia ya kujichukulia sheria mkononi na kwamba wanapaswa kutoa taarifa kwenye vyombo vya usalama iwapo kuna mtu wanamshuku kuwa siyo mwema kwa jamii.

Kadhalika amewataka vijana wanaoendesha vitendo hivyo kutambua kuwa kuzeeka siyo kuwa mchawi na kwamba hata wao ipo siku watazeeka kwa kuwa huo ni mpango wa Mungu na badala yake wanapaswa kufanya kazi kwa bidii ili waboreshe maisha yao kuliko kutegemea mali za wazazi wao.

                                        Mwisho.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni